Featured

RC MAKALLA AZINDU KAMPENI YA ANUANI ZA MAKAZI,ATOA MAAGIZO MAZITO

Written by mzalendoeditor

– Awasihi kuweka jitiada zote kufanikisha Zoezi hilo kalba ya April 15 liwe limekamilika.

– Aelekeza kila Mtaa/Kata kuanzisha Kamati za kuratibu.

– Asema Dar es salaam itatekeleza zoezi hilo kwa ufanisi mkubwa.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Amos Makalla leo amefanya kikao Cha pamoja na Watendaji wa Kata na Mitaa yote ya Dar es salaam na kuwapatia maelekezo ya namna Bora ya kwenda kutekeleza zoezi la Anuani za Makazi ili kupisha Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022.

RC Makalla amesema zoezi hilo ni muhimu na ndio Msingi wa Sensa ya Watu na Makazi ya 2022 hivyo wanatakiwa kuliwekea Mkazo ili kuhakikisha linafanyika kwa umakini na kukamilika kabla ya April 15 2022.

Akizungumza wakati wa kikao hicho kilichojumuisha pia Madiwani na Wenyeviti wa Mitaa, RC Makalla amewataka kuhakikisha Majina ya Mitaa watakayoyachagua yanakuwa ya heshima huku akitahadharisha zoezi lisiwe chanzo Cha Migogoro ya mipaka baina ya Mtaa na Mitaa.

Aidha RC Makalla amesema Serikali inaendelea kushirikiana na Wadau kuhakikisha Vibao vya kuweka kwenye nyumba vinapatikana kwa gharama nafuu ambayo kila Mwananchi ataweza kuimudu.

Hata hivyo RC Makalla amemshukuru na kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wake wa kuleta zoezi hilo linaloifanya Tanzania kuwa na anuani ya kueleweka na hadhi ya kimataifa.

Pamoja na hayo RC Makalla pia amewaelekeza Wenyeviti wa Mitaa Na Kata kuhakikisha wanahitisha kikao na wamiliki wa Hotel, Lodge na Nyumba za Wageni ili kuhakikisha siku ya sensa wageni wote waliolala siku hiyo wanahesabiwa.

Miongoni mwa faida za kuwa na anuani za Makazi ni pamoja na Kupunguza Migogoro ya Ardhi, kuimarisha ulinzi na usalama, kuchagiza biashara mtandao, kusaidia utambuzi wa huduma za kijamii ndani ya eneo husika, kurahisisha kuelekeza mgeni na kuweka mpangilio mzuri wa Jiji.

About the author

mzalendoeditor