Featured Kitaifa

KIHONGOSI:ZAIDI YA WANANCHI MILIONI 45 WAMESHIRIKI KAMPENI ZA URAIS ZA DKT.SAMIA

Written by Alex Sonna

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ndugu Kenani Kihongosi,akizungumza na waandishi wa habari leo Oktoba 5, 2025) katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi Kuu ya CCM jijini Dodoma

Na.Alex Sonna-DODOMA

KATIBU   wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Ndugu Kenani Kihongosi, amesema kuwa tangu kuanza kwa kampeni za Urais kupitia CCM kwa mgombea wake Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, zaidi ya wananchi milioni 45 tayari wameshiriki kwa namna mbalimbali.

Amesema kati ya hao, wananchi milioni 14.6 wamehudhuria mikutano ya kampeni, huku milioni 31.6 wakifuatilia kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, hatua inayoonesha mwitikio mkubwa wa wananchi katika kampeni hizo za mwaka 2025.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Oktoba 5, 2025) katika ukumbi wa mikutano wa Ofisi Kuu ya CCM Dodoma, Kihongosi amesema kuwa uzinduzi wa kampeni ulifanyika kwa kishindo Agosti 28, 2025 katika Uwanja wa Kawe, Dar es Salaam, na uliweka historia kwa kuvunja rekodi ya mahudhurio na shamrashamra tangu kuasisiwa kwa chama hicho.
Ametoa takwimu za kampeni, Kihongosi ameeleza kuwa hadi sasa Dkt. Samia amefanya jumla ya mikutano 77 katika mikoa 21 ya Tanzania Bara na Zanzibar, ikiwemo Kanda ya Kati, Magharibi, Kusini, Nyanda za Juu Kusini, Pwani, Pemba na Unguja.
Amesema wananchi wameendelea kuonesha imani kubwa kwa Dkt. Samia kwa kujitokeza kwa wingi kumsikiliza akinadi Ilani ya Uchaguzi ya CCM (2025–2030), sera na ahadi zake.
Aidha, Kihongosi amebainisha kuwa imani hiyo inachochewa na uongozi wenye mafanikio makubwa uliooneshwa na Dkt. Samia katika kipindi cha miaka minne, mafanikio ambayo yamewapa Watanzania matumaini ya taifa lenye maendeleo, mshikamano na ustawi wa watu wote.

Hata hivyo  Kihongosi,ameongeza kuwa  kampeni hizo zimekuwa za kistaarabu na hazijajikita katika siasa za matusi au kejeli, bali zimebeba ujumbe wa matumaini, mshikamano, na maendeleo jumuishi ya taifa.

Aidha, ameeleza kuwa kuanzia Oktoba 7, 2025, mgombea huyo ataendelea na ziara zake katika mikoa ya Kanda ya Ziwa, ikiwemo Simiyu, Mwanza na Mara, ambapo atazungumza na wananchi katika mikutano ya hadhara, kuwasilisha sera na kuelezea kwa kina dhamira ya CCM ya kuijenga Tanzania ya kisasa na yenye ustawi wa kiuchumi.

“Tunawaomba wananchi waendelee kujitokeza kwa wingi katika mikutano hiyo, wakimsikiliza mgombea wetu ambaye amejidhihirisha kuwa ni kiongozi mwenye dira, busara na uwezo wa kuyaongoza mageuzi ya kiuchumi na kijamii kwa manufaa ya wote,” alisisitiza.

Amehitimisha kwa kusema kuwa CCM itaendelea kuendesha kampeni zake kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, huku ikihimiza amani na mshikamano kwa kila hatua ya mchakato wa uchaguzi.

About the author

Alex Sonna