Na Mwandishi Wetu- Sumbawanga
Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deus Sangu ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kwela amewataka wanachama wa Chama cha Mapinduzi katika Jimbo la Kwela Wilaya ya Sumbawanga Mkoani Rukwa kuwa mstari wa mbele kukisemea Chama hasa kutambua mambo makubwa yaliyofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan
Amesema ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Rukwa, Ujenzi wa Shule ya amali katika Kata ya Munokola, ujenzi wa Barabara za lami pamoja na vituo vya afya ni mifano ya miradi mikubwa inayoendelea kutekelezwa katika jimbo hilo.
Mhe. Sangu ambaye ametoa kauli hiyo kwa nyakati tofauti wakati akizungumza na Wenyeviti, Makatibu na Mabalozi wa CCM wa Kata ya Munokola, Kasanzama na Laela, ikiwa ni muendelezo wake wa ziara ya kimkakati ya kuelezea utekelezaji wa Ilani ya CCM katika Jimbo hilo analoliongoza.
“Mwaka huu ni wa uchaguzi lazima ninyi kama viongozi wa CCM mkisemee chama ili kisonge mbele pia mtambue mazuri yaliyofanywa na Rais Samia hasa katika jimbo letu kwani tumejionea miradi mikubwa ilyotekelezwa ikiwemo ya maji, umeme, Barabara, Shule, vituo vya afya, Madaraja makubwa pamoja na vivuko” amesema Mhe. Sangu
Mhe. Sangu amewataka viongozi hao wa CCM wasiwe wanyonge badala yake wawe mstari wa mbele katika kuyasemea mazuri yaliyofanywa na chama hicho na ikitokea wamekutana na watu wanaobeza chama wawajibu kwa hoja kwa kuwatajia miradi lukuki iliyotekelezwa na inayoendelea kutekelezwa katika jimbo hilo
Mbunge huyo amesema miradi ya maendeleo iliyotekelezwa katika Kata hizo haikuwahi kutokea tangu jimbo hilo kuundwa.
Amesema wanaposema Mama Samia miaka mitano tena, wanasema kwa sababu wanamambo wanayoishi katika Jimbo lao la Kwela.
Aidha Mhe. Sangu ametoa rai Kwa wananchi wa Jimbo lake na taifa Kwa ujumla kwamba waendelee kumuunga mkono Mhe. Dkt. Rais Samia Suluhu Hassan Kwa kazi kubwa anayoifanya katika Taifa la Tanzania na ujasiri anaowapa hasa katika kulipigania Taifa letu