Na Mwandishi Wetu
Familia ya Kichwabuta kutoka Bukoba imeanzisha umoja wa kusaidiana kiuchumi, kielimu na pale mwanaukoo anapopatwa na changamoto na kulinda tamaduni wao.
Umoja huu unalenga kukabiliana na mmong’onyoko wa maadili unaosababishwa na teknolojia na mabadiliko huku pia kujengeana uwezo wa kiufahamu katika kuinuana kiuchumi na kielimu.
Akizungumza jana, Desemba 15,2025 jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Umoja wa Kichwabuta, Creus Kyome, amesema umoja huo umefanikisha kukutanisha wanafamilia kwa lengo la kujadili masuala ya uchumi na maendeleo ya familia.
Kyome alisema, “Lengo letu ni kuimarisha familia na kuhakikisha tunasaidiana kiuchumi na kielimu, lakini pia tunalinda utamaduni wetu ambao umekuwa ukishambuliwa na mabadiliko ya kijamii.”
Kwa Upande wake Katibu wa Umoja wa Kichwabuta, Godfrey Kazinja, amewataka wanaukoo wa Kichwabutwa kote walipo kuungana ili kuimarisha umoja huo na kuleta maendeleo ya pamoja.”
Familia yetu inahitaji kushirikiana zaidi ili kuleta maendeleo, na hili linaweza kufanikishwa tu tukijua kuwa umoja ni nguvu,” alisema Kazinja.
Naye Rosemary Kazinja, ambaye ni Mweka Hazina wa Umoja wa Kichwabuta, amesema kuwa huu ndio wakati muafaka kwa wanafamilia kuungana na kuendeleza familia na tamaduni zao, hasa katika kizazi hiki cha sasa.
“Huu ni wakati wa vijana wetu kuelewa umuhimu wa utamaduni wetu na kuunga mkono juhudi za kuendeleza familia yetu,” alisema Rosemary.
Omari Rulengwa, ni Muhamasishaji wa Umoja wa Kichwabuta, amesema mmong’onyoko wa maadili katika jamii ni janga linalosababishwa na kutofuata mila za ukoo. Ameongeza kuwa umoja huo utaendelea kuhamasisha familia kudumisha maadili ya ukoo.
“Maadili ya familia yetu yameporomoka kwa sababu ya mabadiliko ya kijamii, lakini kwa kushirikiana tunaweza kurudisha maadili na utamaduni wetu,” alisema Rulengwa.
Umoja wa Kichwabuta umejizatiti kuhakikisha unalinda utamaduni na kuendeleza familia kwa kupitia msaada wa kiuchumi na kielimu, na kuhamasisha mshikamano kati ya wanajamii wa kabila hilo.










