Na WMA – DODOMA
Katika siku ya pili ya Maonesho ya Nanenane kitaifa jijini Dodoma, wadau mbalimbali wameonekana kuvutiwa na elimu ya vipimo inayotolewa na Wakala wa Vipimo (WMA) hivyo kuitikia kwa wingi kutembelea Banda hilo.
Tangu mapema asubuhi banda la WMA limekuwa likizungukwa na wakulima, wafugaji, wavuvi na wafanyabiashara wanaotaka kujifunza jinsi ya kutumia na kuhakiki vifaa vya upimaji.
Wataalamu wa WMA wamekuwa wakitoa elimu kuhusu madhara ya vipimo visivyo sahihi na faida ya kutumia vifaa vilivyohakikiwa katika uuzaji wa mbegu, mbolea, maziwa na mazao mengine.
Akizungumza wakati wa kutoa elimu hiyo, Meneja Mawasiliano wa WMA Bi. Veronica Simba alisema mwitikio ni mkubwa kwasababu wadau wameanza kuelewa kuwa kilimo chenye tija kinategemea vipimo sahihi. “Hii inaonyesha watu wanataka kujua na kujikinga na hasara,” alisema.
WMA imesema elimu hii itaendelea kutolewa bure kwa siku zote za maonesho chini ya kaulimbiu “Usahihi wa Vipimo vya Mbegu, Pembejeo, Mazao na Bidhaa Sokoni ni Msingi wa Tija na Utekelezaji wa Dira 2050.”
