Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amekutana na kufanya mazungumzo na na Mkurugenzi Mkaazi wa Benki ya Dunia, anayeziwakilisha pia nchi za Malawi, Zambia na Zimbabwe, Bw. Nathan Belete, katika Ofisi ya Waziri wa Fedha, Treasury Square, jijini Dodoma, ambapo wamejadili kuhusu utekelezaji wa program mbalimbali zinazofadhiliwa na Benki hiyo hapa nchini.
Akizungumza katika kikao hicho, Mhe. Balozi Omar, aliishukuru Benki ya Dunia kwa kuendelea kuwa mshirika muhimu wa maendeleo ya Tanzania na kwamba Serikali inathamini kwa kiwango cha juu uhusiano huo wa muda mrefu, ushirikiano ambao umechangia kwa kiasi kikubwa maendeleo ya nchi kupitia ufadhili wa miradi mbalimbali ya kimkakati ya kiuchumi na kijamii.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkaazi wa Benki ya Dunia, Bw. Nathan Belete, alisema kuwa, Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye miradi mikubwa zaidi inayofadhiliwa na Benki ya Dunia na kupongeza kwa namna inavyotekelezwa kwa ufanisi mkubwa.
Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Kamishna Msaidizi Idara ya Fedha za Nje, Bw. Robert Mtengule, Mwakilishi wa Shirika la Kimataifa la Benki ya Dunia linalohusika na kutoa Mikopo na Misaada ya Kiufundi kwa Sekta Binafsi (IFC), Bi. Martine Valcin, Meneja wa Uendeshaji Mkazi wa Benki hiyo, Bi. Milena Stefanova na maafisa wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha.
