Featured Kitaifa

RAIS DKT.MWINYI ASOMA DUA KABURINI KWA MWANAZUONI MKUBWA WA KIISLAMU

Written by Alex Sonna

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Alhaj Dk. Hussein Ali Mwinyi, amezuru na kusoma dua katika kaburi la Al-Habib Ahmad bin Abubakar bin Sumeit, aliyekuwa mwanazuoni mkubwa wa fani mbalimbali za dini ya Kiislamu na aliwahi kuwa Kadhi Mkuu wa Zanzibar kati ya mwaka 1883 hadi 1886.

Ziara hiyo imefanyika leo, Novemba 7, 2025, katika Msikiti wa Ijumaa Malindi, mara baada ya Dk. Mwinyi kuwasili msikitini hapo kwa ajili ya kushiriki Sala ya Ijumaa.
Katika tukio hilo, Dk. Mwinyi aliungana na viongozi mbalimbali akiwemo Mwalim Haroun Ali Suleiman, Mwakilishi wa Jimbo la Makunduchi; Sheikh Khalid Mfaume, Katibu Mtendaji wa Ofisi ya Mufti Zanzibar; Ustadh Salum Hemed Saleh, Naibu Imamu wa Msikiti wa Ijumaa; na Dk. Abdullah Hasnuu Makame, Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki.
Aidha, Rais Mwinyi amewahimiza wananchi kuendeleza utaratibu wa kuiombea nchi amani, akisisitiza kuwa bila amani, juhudi za Serikali katika kutekeleza mipango ya maendeleo haziwezi kufanikiwa.

Amesema  ni jukumu la kila mwananchi kuhakikisha Tanzania na Zanzibar zinaendelea kuwa visiwa vya amani, umoja na mshikamano, ili kuwezesha utekelezaji wa mipango ya maendeleo kwa mafanikio.

“Tuendelee kuiombea nchi yetu amani, kwani bila amani hakuna maendeleo. Serikali inatekeleza mipango mingi ya maendeleo, hivyo tunapaswa kuiombea Mungu atujaalie utulivu na mshikamano,” amesema Dk. Mwinyi.

Alhaj Dk. Mwinyi amewataka viongozi wa dini kuendeleza juhudi za kuhimiza maadili mema, upendo na mshikamano miongoni mwa wananchi, ili kuijenga jamii yenye maadili na inayomcha Mungu.

AHMED ABDUL-SHAKUR ABDALLA
(IKULU ZANZIBAR)

About the author

Alex Sonna