Featured Kitaifa

DKT. SAMIA AAHIDI UJENZI WA UWANJA WA NDEGE MISSENYI MKOANI KAGERA

Written by Alex Sonna
Mgombea wa nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema ikiwa atapewa ridhaa ya kuunda serikali kupitia Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, ataanza ujenzi wa uwanja wa ndege eneo la Kyabajwa katika Wilaya ya Misenyi, mkoani Kagera,uwanja utakaokuwa na uwezo wa kuhudumia ndege kubwa ikiwemo ndege za abiria zenye uwezo wa kubeba abiria 180 mpaka abiria 220.

Mbele ya maelfu ya wanachama wa Chama chake na wananchi wa Missenyi leo Jumatano Oktoba 15, 2025, katika mkutano wa kampeni uliofanyika Kyaka, Dkt. Samia amesema kuwa uwanja huo mkubwa na wa kisasa unatarajiwa kufungua fursa mpya za uwekezaji na kukuza sekta ya utalii, biashara na kilimo biashara ndani ya mkoa wa Kagera na maeneo jirani.

“Tumeanza kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujenga uwanja mkubwa na wa kisasa katika eneo la Kyabajwa. Awali, ilipendekezwa Omukajunguti, lakini eneo hilo halikufaulu vizuri katika upembuzi yakinifu, hivyo tumeamua kujenga Kyabajwa.” Amesema Dkt. Samia.

Kulingana na Dkt. Samia, uwanja huo utakuwa na uwezo wa kuhudumia ndege kubwa za kimataifa kama Boeing 737-900, zenye uwezo wa kubeba abiria 180 hadi 220, jambo litakalofungua milango ya kiuchumi na fursa za biashara kwa wananchi wa Missenyi na maeneo ya mpakani mwa Tanzania na Uganda.

Ameongeza kuwa mradi huo ni sehemu ya juhudi za serikali za kuimarisha miundombinu ya usafiri na kusukuma mbele sera ya kilimo biashara, kwa kuwezesha usafirishaji wa mazao na bidhaa za kibiashara kwenda ndani na nje ya nchi.

About the author

Alex Sonna