Featured Michezo

UBABE WA YANGA WAENDELEA,YAICHAPA SIMBA SC MARA SITA MFULULIZO

Written by Alex Sonna

Yanga SC chini ya Kocha Mkuu, Romain Folz, imetwaa taji la Ngao ya Jamii baada ya kuibuka na ushindi  wa bao 1-0 dhidi ya watani wao wa jadi, Simba SC, katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.

Bao pekee la ushindi kwa Yanga SC limefungwa na Pacome Pacome Zouzoua  dakika ya 53 akiwa ndani ya 18 akimfunga kipa Moussa Camara.

Yanga SC wameanza msimu wa 2025/26 wakitwaa taji ambalo walikuwa wanalitetea baada ya kutwaa msimu wa 2024/25 kwa kuwafunga mabao 4-1 Azam FC.

Simba SC haijawa na bahati mbele ya Yanga SC kwa kuwa msimu wa 2024/25 katika mechi tatu walizokutana uwanjani walipoteza.

Kwa mara nyingine tena Yanga SC wameendeleza ubabe wao kwa kupata ushindi ikiwa ni mara ya sita mfululizo mbele ya Simba SC inayonolewa na Kocha Mkuu, Fadlu Davids.

Katika mchezo huo, washambuliaji wa Simba, Kibu Dennis na Ellie Mpanzu, walipoteza nafasi kadhaa za wazi katika kipindi cha kwanza, hali iliyowapa wakati mgumu hadi mwisho wa mchezo.

About the author

Alex Sonna