Mamlaka ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala (THBUB) ni kulinda na kukuza haki za binadamu na misingi ya utawala bora nchini.
Hayo amesema Kamishna wa THBUB Mhe. Dkt.Thomas Masanja wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Banda la THBUB kwenye Maonesho ya Kimataifa ya Biashara ‘Sabasaba’ Julai 1, 2025 Jijini Dar Es Salaam.
Mhe. Dkt. Masanja amesema kuwa THBUB inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Ibara ya 130 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Kifungu cha 6(1) cha Sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Sura ya 391.
“Katika kulinda haki za binadamu na misingi ya utawala bora pia THBUB inafanya uchunguzi wa malalamiko yanayohusiana na uvunjwaji wa haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora” amesema Mhe. Dkt. Masanja
Aidha, Mhe. Dkt. Masanja amesema kuwa THBUB ina jukumu la kuishauri Serikali katika masuala yote yanayohusu haki za binadamu na utawala bora.
” Sisi kama washauri wa Serikali hatutakiwi kulalamika bali ikitokea mamlaka fulani inalalamikiwa basi THBUB inajukumu la kutoa mapendekezo ya juu kinacholalamikiwa” amesema Mhe. Dkt.Thomas Masanja.
Wakati huo huo Mhe. Dkt. Thomas Masanja ametoa wito kwa wananchi wa Jiji la Dar Es Salaam na Mikoa ya jirani Kufika katika Banda la THBUB kwenye Maonesho ya Kimataifa ya Biashara yanayoendelea katika Viwanja vya Mwl. Julius Kambarage Nyerere Jijini Dar es Salam ili kupata huduma mbalimbali zikiwemo elimu ya haki za binadamu na utawala bora, kupata msaada wa kisheria bure, kuwasilisha na kufuatilia malalamiko yao sambamba na kuifahamu THBUB.