Featured Kitaifa

TSN YATOA WITO KWA TAASISI KUSHIRIKIANA KATIKA UTUNZAJI KUMBUKUMBU

Written by mzalendoeditor
Na Alex Sonna, Dodoma
Afisa Uhusiano wa Kampuni ya Magazeti ya Serikali (Tanzania Standard Newspapers – TSN),  Nadhifa Omary, amesema kampuni hiyo inayochapisha magazeti ya HabariLEO na Daily News inaendelea kutoa mchango mkubwa katika uhifadhi wa taarifa na kumbukumbu muhimu kwa maendeleo ya taifa.
Ameeleza kuwa mbali na shughuli za uchapishaji wa magazeti, TSN pia inajihusisha na uchapishaji wa nyaraka mbalimbali kama vile kalenda, diary, vitabu na machapisho mengine ya serikali na taasisi binafsi.
“TSN ni kampuni kongwe inayohifadhi kumbukumbu nyingi za viongozi na matukio muhimu ya taifa kwa ajili ya vizazi vijavyo,tunajua baadhi ya taasisi mpya bado hazina mfumo madhubuti wa kuhifadhi kumbukumbu, hivyo tunawakaribisha kushirikiana nasi ili kulinda historia ya nchi yetu,” amesema Nadhifa.
Aidha, ameeleza kuwa Serikali imeendelea kuiboresha kampuni hiyo kwa kuipatia mtambo mpya wa kisasa unaowezesha kazi kufanyika kwa haraka na kwa viwango vya juu vya ufanisi, jambo linaloiwezesha TSN kwenda sambamba na teknolojia ya kisasa katika tasnia ya habari na uchapishaji.
Akizungumzia ushiriki wa TSN kwenye maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma, yenye kaulimbiu “Himiza Matumizi ya Mifumo ya Kidijitali, Ongeza Upatikanaji wa Taarifa na Kuchochea Uwajibikaji katika Utumishi wa Umma,” amesema maonesho hayo yamekuwa fursa ya kipekee kwao kukutana na wananchi mbalimbali na kuwaelimisha kuhusu majukumu na huduma zinazotolewa na ofisi yao.
“Tumeweza kueleza kwa kina namna tunavyofanya kazi, huduma tunazotoa na pia tumepokea mrejesho mzuri kutoka kwa wananchi waliotembelea banda letu,” ameongeza.

About the author

mzalendoeditor