Featured Kitaifa

WIZARA YA ULINZI YAJIVUNIA KUTATUA MIGOGORO YA ARDHI NA KULIPA FIDIA

Written by mzalendoeditor

WAZIRI wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Stergomena Tax, akizungumza na waandishi wa habari  kuhusu mafanikio ya Wizara hiyo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan leo Mei 22,2025 jijini Dodoma

Na.Alex Sonna-DODOMA

KATIKA  kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita,Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa,imefanikiwa kutatua migogoro ya ardhi iliyotambuliwa kwa kuhuisha mipaka, kupima maeneo, kufanya uthamini na kulipa fidia katika baadhi ya maeneo ya wananchi wanaostahili.

Hayo yameelezwa leo Mei 22,2025 jijini Dodoma na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Stergomena Tax,wakati akizungumza na waandishi wa habari  kuhusu mafanikio ya Wizara hiyo katika kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Katika kipindi cha miaka minne kuanzia Mwaka wa Fedha 2020/21 hadi kufikia Februari 2025, wizara imefanikiwa kutatua migogogro ya ardhi 80 kwa kupima maeneo 263 na kuyapatia hati miliki maeneo 143. Aidha, wizara imefanikiwa kufanya tathmini na kulipa fidia jumla ya maeneo 61 yenye gharama ya Sh. 54,130,521,088.81,”amesema Waziri Dkt.Tax

Aidha ametaja mafaniko mengine katika sekta ya ulinzi kwa kipindi hicho cha miaka minne ni pamoja na ujenzi na ulinzi wa miradi mbalimbali ya kimkakati.

 

Dkt.Tax amesema kuwa miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa Ikulu ya Chamwino Dodoma, ulinzi wa Reli ya Kisasa (SGR), ulinzi wa mradi wa kufua Umeme wa Maji wa Julius Nyerere, ulinzi wa mgodi wa Tanzanite uliopo Mirerani mkoani Manyara.

 

Pia, ulinzi katika bomba la kusafirisha mafuta ghafi kutokea nchini Uganda hadi mkoani Tanga, ulinzi wa mradi wa kuchakata gesi asilia Likong’o mkoani Lindi na kivuko cha Busisi, ulinzi katika Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) hasa Bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara, ulinzi wa Kampuni ya Simu (TTCL), ulinzi wa  Viwanja vya Ndege na Uundaji wa meli katika Ziwa Victoria.

 

“Mafanikio hayo yamechangia katika kukuza uchumi na kuimarisha ulinzi, hususan katika maeneo ya kimkakati ambayo hayana budi kusimamiwa na Taasisi zitakazolinda maslahi ya Taifa. Hii imewezekana kutokana na uongozi mahiri wa Serikali ya Awamu ya sita,”amesema 

Aidha, kupitia JWTZ, Serikali imekabidhiwa jukumu la kujenga nyumba 5,000 kwa wananchi waliokubali kuhama kwa hiari kutoka Ngorongoro ambapo hadi sasa, nyumba 2,500 zimekamilika katika eneo la Msomera – Handeni, huku nyingine 1,000 zikijengwa Sauni – Kilindi na 1,500 zikitarajiwa kujengwa Kitwai B – Simanjiro, Manyara.
Kwa upande wa Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Kujenga Taifa (SUMAJKT) katika kuendeleza uchumi na kupunguza mzigo wa gharama kwa serikali, Dk. Tax amesema  limechangia jumla ya Shilingi bilioni 2.67 kwa ajili ya malezi ya vijana wa JKT na kutoa gawio la zaidi ya Shilingi bilioni 4.27 kwa Serikali kupitia Hazina.
Miongoni mwa miradi ya kiuchumi iliyoanzishwa ni pamoja na vituo vya madini mikoa saba ikiwemo Tanga, Ruvuma, na Mara,ujenzi wa majengo ya halmashauri na taasisi za serikali,Viwanda mbalimbali ikiwemo vya maji, mavazi, bidhaa za ngozi, na taa za LED,Usambazaji na ufungaji wa umeme vijijini kupitia mradi wa REA,usambazaji wa matrekta na zana za kilimo katika mikoa zaidi ya 10 na huduma ya ulinzi kwa taasisi nyeti kupitia kampuni ya SUMAJKT Guard.
Aidha amesema kuwa  mafanikio hayo ni matokeo ya usimamizi madhubuti na dhamira ya serikali katika kujenga nchi inayojitegemea kiusalama na kiuchumi kupitia taasisi zake za kijeshi.
Hata hivyo amesema kuwa JWTZ  limehusika katika zaidi ya shughuli sita kubwa za uokoaji ndani na nje ya nchi, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kushirikiana na mamlaka za kiraia kukabiliana na majanga na maafa mbalimbali.
“Tumeimarisha uwezo wa JWTZ katika shughuli za kukabiliana na majanga. Kwa kipindi cha miaka minne, tumeshiriki kikamilifu kwenye matukio makubwa ya maafa kwa kutoa misaada ya uokoaji na kibinadamu,” amesema  Dk. Tax.
Ameyataja miongoni mwa matukio hayo ni uokoaji katika mafuriko ya Mtwara,kuzima moto katika Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro,usafirisha misaada na kuokoa wahanga wa mafuriko nchini Malawi,uokoaji katika maporomoko ya matope Hanang’ – Manyara,kuokoa waliopata ajali ya jengo Kariakoo – Dar es Salaam na ujenzi wa nyumba kwa waathirika wa Hanang’ na wakazi waliopisha uhifadhi Ngorongoro waliohamishiwa Tanga.

About the author

mzalendoeditor