Featured Kitaifa

DKT.MFAUME: TAMISEMI TUMEJIPANGA VYEMA UTEKELEZAJI WA SHERIA YA BIMA YA AFYA KWA WOTE

Written by mzalendoeditor

OR-TAMISEMI

Mkurugenzi wa Idara ya Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI, Dkt. Rashid Mfaume, amesema kuwa katika kuelekea utekelezaji wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, TAMISEMI imejipanga vyema kuhakikisha kunakuwa na usimamizi bora huduma za afya katika ngazi ya msingi.

Dkt. Mfaume ametoa kauli hiyo alipokuwa katika ziara yake ya kukagua utoaji wa huduma za afya, lishe, na ustawi wa jamii mkoani Dodoma, ambapo alitembelea Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa.

Amesema TAMISEMI itahakikisha katika ngazi ya afya ya msingi bidhaa zote muhimu za afya zinapatikana.

“Tunawahakikishia Watanzania kuwa katika ngazi ya huduma za afya ya msingi, Ofisi ya Rais TAMISEMI imejipanga kuhakikisha wananchi wote wanaojiunga na Bima ya Afya kwa Wote wanapata huduma zote stahiki kama inavyotakiwa,” amesema Dkt. Mfaume.

Aidha, amebainisha kuwa hapo awali kulikuwapo na changamoto ya baadhi ya wanachama wa bima ya afya kukosa dawa katika vituo vya kutolea huduma na kulazimika kununua dawa hizo wenyewe.
Hata hivyo, kwa sasa TAMISEMI imechukua hatua kuhakikisha vituo vya afya vinakuwa na akiba ya kutosha ya dawa na vifaa tiba ili kuboresha huduma kwa wananchi.

About the author

mzalendoeditor