Featured Kitaifa

WAZIRI SIMBACHAWENE ASHIRIKI IBADA YA SHUKRANI YA ALIYEKUWA WAZIRI MKUU, HAYATI EDWARD LOWASSA, ASISITIZA SUALA LA AMANI

Written by mzalendoeditor

Na Lusungu Helela-MONDULI

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene amewataka Watanzania kumuenzi aliyekuwa Waziri Mkuu, Hayati Edward Lowassa kwa kuendelea kudumisha umoja, amani na mshikamano ili kuepuka mapigano yanayoendelea katika nchi zingine.

Mhe. Simbachawene ametoa kauli hiyo leo Jumapili Februari 9, 2025 wakati wa Ibada maalumu ya Kumbukizi ya mwaka mmoja wa aliyekuwa Waziri Mkuu wa Tanzania, Hayati Edward Lowassa huku akiwataka Watanzania kuendeleza yale yote mazuri aliyokuwa akiyafanya.

Aidha, Mhe. Simbachawene amesema Hayati Edward Lowassa atakumbukwa daima kwa kuwagusa watu wengi kwa namna chanya.

Amefafanua kuwa Hayati Edward Lowassa ni Kiongozi aliyekuwa na upendo, aliyewasaidia watu wengi na aliyependa kuzungumza na kila mtu bila kujali anamfahamu au hamfahamu.

Ameongeza kuwa “Hayati Edward Lowassa ni kiongozi aliyekuwa hapendi kumuona mtu yeyote akipata shida, alitamani kumuona kila mmoja akiwa na furaha wakati wote” amesema.

Katika hatua nyingine Mhe. Simbachawene amemshukuru Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kumuenzi Hayati Lowassa kwa mchango wake chanya aliokuwa akiutoa kwa maendeleo ya taifa.

“Hivi sasa tuna shule nyingi zimejengwa na zimeendelea kujengwa, barabara, miradi ya maji imeendelea kutekelezwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan” ameongeza.

Akizungumza kwa niaba ya Familia ya Hayati Edward Lowassa, mtoto wa kwanza ambaye pia ni Mbunge wa Monduli, Mhe. Fredrick Lowassa ametumia fursa hiyo kuwashukuru wote waliokuwa pamoja tangu baba yao alipofariki hadi hivi sasa huku akimtaja Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake mkubwa kwa familia hiyo tangu baba yao alipoanza kuugua hadi umauti ulipomkuta.

“Ikiwa leo ni mwaka mmoja tangu baba yetu atutoke, alikuwa ni kiongozi na nembo ya Wananchi wa Monduli, tuendelee kumuenzi kwa mchango wake mkubwa katika kudumisha mshikamano kwa jamii za wafugaji wa asili” amesisitiza Mhe. Fredrick Lowassa

Aidha, Ametumia fursa hiyo kuiomba Serikali iharakishe mchakato wa kuandaa Makumbusho ya Hayati Edward Lowassa kutokana na ujio wa wageni wengi wanaofika nyumbani hapo kwa ajili ya kujifunza mambo aliyokuwa akiyafanya baba yao.

Naye, Baba Askofu Mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la kilutheri Tanzania KKKT Dayosisi ya Kaskazini Kati, Dkt. Solomon Masangwa ameisisitiza familia ya Hayati Edward Lowassa kuzidi kumshirikisha Mungu katika kila jambo wanalolifanya ili kuendelea kushikamana.
Hayati Edward Ngoyai Lowassa alifariki dunia Februari 10, 2024 na kuzikwa nyumbani kwake Monduli tarehe 17 Februari 2024.

  

Mbunge wa Monduli, Mhe. Fredrick Lowassa akisalimiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe.George Simbachawene wakati wa Ibada ya Shukrani ya aliyekuwa Waziri Mkuu Mstaafu Hayati Edward Ngoyai Lowassa iliyofanyika leo katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Monduli Mjini Mkoani Arusha.

Sehemu ya wanafamilia wa Hayati Edward Lowassa wakiwa kwenye Ibada ya Shukrani ya aliyekuwa Waziri Mkuu Mstaafu, Hayati Edward Ngoyai Lowassa iliyofanyika leo katika Kanisa la Kiinjili Kilutheri Tanzania (KKKT) Monduli Mjini Mkoani Arusha.

Baadhi ya wananchi wakiwa katika Ibada ya Shukrani ya aliyekuwa Waziri Mkuu Mstaafu Hayati Edward Ngoyai Lowassa iliyofanyika leo katika Kanisa la Kiinjili Kilutheri la Tanzania (KKKT) Monduli Mjini Mkoani Arusha.

About the author

mzalendoeditor