Featured Kimataifa

TANZANIA NA UINGEREZA ZASAINI MKATABA WA USHIRIKIANO WA MIAKA MITANO

Written by mzalendo
WAZIRI   wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof.Kitila Mkumbo,akiwa na Waziri wa Uingereza wa Maendeleo na Afrika Andrew Mitchell,(waliosimama) wakishuhudia utiaji saini wa mkataba wa ushirikiano kwa ajili ya ustawi wa Tanzania na Uingereza, wakisaini Mkataba huo ni Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji  Dk.Tausi Kida na Balozi wa Uingereza nchini David Concar (Waliokaa), hafla hiyo imefanyika leo Aprili 5,2024 jijini Dodoma.
Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji  Dk.Tausi Kida na Balozi wa Uingereza nchini David Concar wakibadilishana Mkataba wa ushirikiano kwa ajili ya ustawi wa Tanzania na Uingereza, hafla hiyo imefanyika leo Aprili 5,2024 jijini Dodoma.
Ujumbe wa Tanzania (kulia) ukiongozwa na Waziri  wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof.Kitila Mkumbo, na Ujumbe wa Serikali ya Uingereza (kushoto) ulioongozwa na Waziri wa Uingereza wa Maendeleo na Afrika Andrew Mitchell, wakifanya mazungumzo kuhusu ushirikiano wa nchi hizo mbili katika nyanja za kukuza maendeleo katika sekta za afya, uwekezaji wa kijamii na ukuaji wa uchumi jumuishi, jijini Dodoma. 
Waziri  wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof.Kitila Mkumbo, akizungumza wakati wa Mkutano na Waziri wa Uingereza wa Maendeleo na Afrika Andrew Mitchell, (hayupo pichani) aliyeambatana na ujumbe wake, ambapo wamefanya mazungumzo kuhusu ushirikiano wa nchi hizo mbili.jijini Dodoma.
Waziri wa Uingereza wa Maendeleo na Afrika Andrew Mitchell, akiwa ameambatana na ujumbe wake wakimsikiliza Waziri  wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof.Kitila Mkumbo (hayupo pichani) wakati wa Mkutano wao  kuhusu ushirikiano wa nchi hizo mbili.jijini Dodoma.
Na.Alex Sonna-DODOMA 
SERIKALI ya Tanzania  na Uingereza  zimesaini mkataba wa makubaliano wa ushirikiano wa miaka mitano wenye thamani ya Sh.Trilioni tatu unaolenga kukuza maendeleo katika sekta za afya, uwekezaji wa kijamii na ukuaji wa uchumi jumuishi.
Akizungumza katika hafla hiyo, leo Aprili 5,2024 jijini Dodoma  Waziri  wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, Prof.Kitila Mkumbo, amesema katika mkataba huo eneo la kuchochea biashara na uwekezaji zitatolewa sh.Bilioni 300.
“Leo nimekutana na Waziri wa Uingereza wa Maendeleo na Afrika Andrew Mitchell, tumeshuhudia utiaji saini wa mkataba wa ushirikiano kwa ajili ya ustawi kati ya Tanzania na Uingereza ambao umesainiwa kati ya Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji  Dk.Tausi Kida na Balozi wa Uingereza nchini David Concar na katika maeneo haya ya biashara na uwekezaji tunatarajia zipatikane Paundi za Uingereza Milioni 100 sawa na Sh.Bilioni 300,”amesema Prof.Mkumbo
Aidha amesema kuwa  katika mkataba huo Tanzania itashirikiana na Uingereza kufanya uwekezaji kwenye madini ya kimkakati, utajikita katika kuongeza thamani hapa hapa nchini.
“Lengo la Rais Samia Suluhu Hassan ambalo amelisukuma sana ni kuongeza thamani mazao yetu ya madini hususan madini ya kimkakati ambayo yanahitajika sana kwenye Green environment katika kutengeneza betri, kwa hiyo jambo hili tumelipokea vizuri kwasababu linalenga kwenda kutuongezea uwezo wetu sisi wenyewe,”amesisitiza

     

About the author

mzalendo