Na.Bolgas Odilo-Mzalendo blog
WAWAKILISHI wa Tanzania katika Mashindano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika Timu ya Yanga SC imetinga hatua ya Robo Fainali ya Michuano hiyo baada ya kuichapa mabao 2-0 US Monastir kutoka nchini Tunisia Mchezo wa Kundi D uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.
Licha ya kunyesha Mvua haikuweze kuwazuia Yanga kuibuka na ushindi kwenye mchezo huo muhimu huku Mashabiki wakifurika kwa wingi ili kuipa sapoti timu yao.
Mshambuliaji kutoka nchini Zambia Kennedy Musonda aliwanyanyua wananchi dakika ya 33 akifunga bao kwa kichwa akimalizia pasi ya Jesus Moloko bao lililowapeleka Yanga mapumziko wakiwa mbele.
Kipindi cha pili timu zote zilifanya mabadiliko ili kuendelea kujimarisha zaidi mnamo dakika ya 58 Fiston Mayele alipigilia msumari wa pili akipokea pasi ya Kennedy Musonda.
Kwa matokeo hayo Yanga SC wamefikisha Pointi 10 na kuongoza kundi D wakilingana na US Monastir wakiwa na uwiano wa mabao ya kufungwa na kufunga tofauti,Real Bamako nafasi ya tatu wakiwa na Pointi 5 huku TP Mazembe wakiburuza mkia kwa Pointi zao tatu.
Tanzania kwa mara ya kwanza inaandika historia kwa kupelekea timu mbili katika mashindano ya CAF baada ya jana Simba SC kutinga Robo Fainali ya Klabu Bingwa Afrika kwa kishindo kuichapa Horoya mabao 7-0.
Mchezo mwingine wa kundi hilo Real Bamako imeichapa mabao 2-1 TP Mazembe mchezo uliopigwa nchini Mali.