Featured Kitaifa

YAKUBU ARIDHISHWA NA MAENDELEO YA UJENZI JENGO LA WIZARA YA UTAMADUNI,SANAA NA MICHEZO

Written by mzalendoeditor

Na Shamimu Nyaki – WUSM

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Saidi Yakubu ameridhishwa na kasi inayoendelea ya ujenzi wa  Jengo la kudumu la wizara hiyo.

Akizungumza alipotembelea eneo la ujenzi Julai 19, 2022 Mji wa Serikali  Dodoma, Bw. Yakubu amempongeza Mkandarasi Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwa kuongeza kasi pamoja na Idadi ya wafanyakazi ambao umechagiza hatua ya kuridhisha katika ujenzi

“Leo kazi inaonekana, mmepiga hatua, nimeona idadi ya wafanyakazi imeongezeka, vifaa vya ujenzi vipo vya kutosha pamoja na malighafi nyingine”alisema Bw.Yakubu.

Aidha, amesisitiza Mkandarasi huyo kuongeza usalama maeneo ambayo yanachangamoto ili watu wasijekuumia, pamoja na kuhakikisha eneo la kupanda miti pamoja na maua linaonekana haraka iwezekanavyo ili miti na maua yapandwe kama alivyoelekeza Waziri wa  Mkuu wa Tanzania  Mhe. Kassim Majaliwa.

Kwa upande wake Mkandarasi wa Jengo hilo Ahmad Abdalah amesema amepokea maelekezo yote na pongezi alizotoa Naibu Katibu Mkuu, ambapo ameahidi kukamilisha ujenzi huo mwezi Oktoba 2023.

Jengo hilo  lenye ghorofa sita kwa sasa limefikia asilimia 30 ya ujenzi na linatarajiwa kuwa na kumbi za mikutano ya ndani, sehemu za michezo na matanki ya maji yenye  ujazo wa lita milioni nne pamoja na eneo la kupumzikia.

About the author

mzalendoeditor