Featured Kitaifa

NHIF TANGA WAELEZEA TIJA YA UANZISHWAJI WA VIFURUSHI VIPYA VYA UANACHAMA

Written by mzalendoeditor


Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga, Ali Mwakababu akizungumza na waandishi wa habari ambao hawapo pichani kwenye banda lao
NA OSCAR ASSENGA,TANGA.

MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya Mkoani Tanga (NHIF)Mkoani Tanga umeelezwa kwamba uanzishwaji wa vifurushi vipya vya uanachama vinavyoruhusu watu wengine tofauti na walioajiriwa katika sekta ya Umma kunufaika na bima ya afya umesaidia ongezeko la wanachama.

Hayo yalisemwa na Meneja wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Tanga, Ali Mwakababu wakati wa maonyesho ya 9 ya Biashara na Utalii yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwahako Jijini Tanga ambapo alisema kuwa idadi ya wananchama wa mfuko huo mkoani Tanga ni zaidi ya 12,000.

Mwakababu alisema hapo awali watu wengi walifikiria mfuko huo ni kwa ajili ya watumishi wa umma pekee lakini umechukua hatua za kuanzisha vifurushi ambavyo vinawavutiwa watu katika Maonyesho ya Biashara ya siku 10 yaliyofunguliwa huko katika viwanja vya Mwahako siku tano zilizopita.

Meneja huyo alisema wananchi wengi ambao wametembelea banda lao wameonyesha nia ya kweli kutaka kujiunga na mfuko ili kuweza kunufika na huduma mbalimbali zinazotolewa ikiwemo kupata matibabu wanapokuwa wakiugua.

Hata hivyo alisema mpaka sasa tayari wametoa elimu kwa zaidi ya wananchi 150 ya ufahamu ya bima ya afya siku tatu za kwanza za maoyesho hayo na tayari baadhi yao wamejaza fomu za kujiunga na mfuko huo.

Alivitaja vifurushi hivyo kuwa ni pamoja na Najali, Wekeza na Timiza Vifurushi vya bima ya afya.

Akizungumza hasa kuhusu ushiriki wa Maonyesho ya Biashara ya NHIF, Ofisa Bima ya Afya, Hussein Mponda alisema kuwa Banda la NHIF ni moja ya banda ambalo linavuta watu wengi wanaomiminika kwenye Maonyesho hayo ya Biashara.

Alisema wengi wanaofika kwenye banda lao wanaulizia jinsi wanaweza kujiunga na mpango wa bima ya afya, mbali na kupata uchunguzi wa matibabu bure.

Hata hivyo aliwahamasisha wananchi kuweza kufika kwenye banda lao ili kuweza kupata huduma mbalimbali ikiwemo za upimaji wa afya na kujiunga na bima ya afya waweze kunufaika na huduma za matibabu pindi wanapougua.

About the author

mzalendoeditor