Featured Kitaifa

WATUMISHI OFISI YA WAKILI MKUU WA SERIKALI WASHIRIKI SHEREHE ZA MEI MOSI DODOMA

Written by mzalendoeditor
Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali leo Tarehe 01/05/2022, imeungana na Wafanyakazi Duniani kote katika kuadhimisha Siku ya Wafanyakazi Duniani “Mei Mosi” yaliyofanyika katika viwanja vya Jamhuri jijini Dodoma.
Watumishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali wakiongozwa na Mwenyekiti wa Tughe Tawi la Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali Mtani Songorwa, wameshiriki Maadhimisho hayo kitaifa kwa kuanza na maandamano yaliyopita mbele ya Mgeni Rasmi wakiwa na Mabango yenye jumbe mbalimbali zinazolenga kuonyesha mshikamano baina ya Watumishi, Vyama vya Wafanyakazi na Serikali yakisindikizwa na kauli mbiu isemayo “Mishahara na Maslahi Bora kwa Wafanyakazi ndio Kilio chetu: Kazi iendelee”.
Mgeni Rasmi wa Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi “Mei Mosi” Mwaka huu ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, ambapo kupitia Maadhimisho hayo ameahidi kuendelea kushughulikia changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi nchini kwa lengo la kuboresha mazingira yao ya kazi.
Aidha, kuhusu kuboresha Maslahi ya watumishi, Mheshimiwa Rais ameziagiza Taasisi husika kuziwezesha kamati ziliyoundwa kushughulikia masuala hayo ili iweze kufanya kazi kikamilifu.

About the author

mzalendoeditor