Featured Kitaifa

MAJALIWA AZIPA MAAGIZO WIZARA UENDELEZAJI KIJIJI CHA MSOMERA, HANDENI

Written by mzalendoeditor

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua ujenzi wa madarsa ya Shule ya Msingi katika kijiji cha Msomera  wilayani Handeni Mkoa wa Tanga kwa ajili ya wananchi walioridhia kuhama katika Hifadhi ya Ngorongoro kwenda kujishi katika kijiji hicho, Aprili 24, 2022. Kulia kwake ni Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga na  na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongella.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua moja kati ya nyumba 103 zinazojengwa na serikali katika kijiji cha Msomera  wilayani Handeni Mkoa wa Tanga kwa ajili ya wananchi walioridhia kuhama katika Hifadhi ya Ngorongoro kwenda kuishi katika kijiji hicho, Aprili 24, 2022. Kulia kwake ni Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga   na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongella. 

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua moja kati ya nyumba 103 zinazojengwa na serikali katika kijiji cha Msomera  wilayani Handeni Mkoa wa Tanga kwa ajili ya wananchi walioridhia kuhama katika Hifadhi ya Ngorongoro kwenda kuishi katika kijiji hicho, Aprili 24, 2022. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

………………………………………..

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa maeitaka Wizara ya Maliasili na Utalii kuendelea kusimamia kwa ukaribu na kuhakikisha shughuli za ujenzi katika kijiji cha Msomera kilichopo Handeni Makoani Tanga zinakamilika haraka.

Amesema kuwa Wizara hiyo inapaswa kuhakikisha inaendelea kutoa elimu kwa wakazi wa Ngorongoro waliojiandikisha kuhama kwa hiari. “Zoezi hili linaloendea la kuimarisha miondombinu ikiwemo upimaji wa viwanja litawanufaisha wakazi wa Msomera pamoja na hao wanaohamia eneo hili.”

Waziri Mkuu ameyasema hayo jana (Jumapili, Aprili 24, 2022) alipokagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali katika kijiji cha Msomera kilichopo Handeni Makoani Tanga kwa ajili ya wakazi wa Ngorongoro waliokubali kuhamia kwenye Kijiji hicho ili kupisha shughuli za uhifadhi kwa maendeleo ya Taifa.

Aidha, Waziri Mkuu ameitaka Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuendelea kuandaa mazingira mazuri ya ufugaji. “Wizara hii inapaswa pia kuhakikisha kwamba kunakuwa na miundombinu wezeshi ya wafugaji yakiwemo malambo ya kunyweshea mifugo, majosho, ujenzi wa kliniki ya kutibu magonjwa ya mifugo katika eneo hilo.”

Akitoa maelekezo kwa Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Mheshimiwa Majaliwa ameitaka iendelee kuwekeza nguvu katika kuimarisha miundombinu ya elimu. “Kama tunavyoona hapa shule ya msingi inajengwa, sekondari inajengwa, zahanati zinakarabatiwa lakini pia ujenzi wa kituo cha afya na barabara unaendelea, ongezeni nguvu.”

Mheshimiwa Majaliwa pia ameitaka Wizara ya Maji iendelee kuhakikisha kiwango cha maji katika eneo hilo kinakuwa toshelevu kwa kuchimba zaidi ili hata majosho na malambo yapate maji ya kutosha. Maji ambayo tayari yameshachimbwa na kuyapata ni mengi kuliko mahitaji lakini tuongeze kiwango.”

Pia, Waziri Mkuu alisema kuwa Watumishi wote wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA) waliojenga katika hifadhi ya Ngorongoro hawataingia kwenye utaratibu wa kupewa nyumba kwa kuwa walivunja sheria. “Nataka niwaambie watumishi wa NCAA mliojenga kule, tutaondoa nyumba zenu zote kwasababu mmevunja sheria, kama unajua umejenga anza kuondoka mwenyewe”.

Kwa upande wake Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Angelina Mabula amesema kuwa Wizara ilipokea shilingi milioni 321 kwa ajili ya kufanya mpango wa matumizi bora ya ardhi katika kijiji cha Msomera na mpaka sasa jumla ya michoro 11 imeshakamilika ambapo michoro mitano tayari ina viwanja 14,250 na katika hivyo viwanja 5,250 tayari viko kamili.

Ameongeza kuwa wakazi hao watapewa viwanja hivyo bure. “Tunatarajia kijiji hiki kitakuwa cha mfano na hata vijiji vingine vitakuja kujifunza hapa. Tulichokifanya kama Wizara ni kuhakikisha mpango wa matumizi bora unakamilika.”

Naye, Waziri wa Jumaa Aweso amesema kuwa Wizara hiyo itahakikisha miradi yote ya maji katika kijiji cha Msomera inakamilika kwa wakati ili wakazi hao waweze kupata huduma ya maji safi na salama.

“Kupitia Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) tunakwenda kuchimba bwawa ambalo litakuwa na uwezo wa kuhifadhi maji lita milioni 700 na tayari tumekamilisha hatua za manunuzi na mkataba imeshasainiwa tumeshaleta shilingi milioni 300 ili kazi iendelee na wakandarasi wote wa Wizarani wapo hapa.”

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki amesema kuwa Serikali imeshatoa fedha kwa ajili ya uejnzi wa majosho mawili mapya na ukarabati wa josho moja lililopo katika kijiji hicho. “ Tunazo pesa na tayari wataalam wetu wapo hapa wapo tayari kushikiana nanyi ili kubaini ni wapi mnataka majosho hayo yajengwe.”

About the author

mzalendoeditor