Featured Kitaifa

SERIKALI KUSHIRIKIANA NA WADAU MAPAMBANO DHIDI YA DAWA ZA KULEVYA NCHINI

Written by mzalendo

Na Mwandishi wetu- Dodoma

Serikali imeahidi kuendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo katika mapambano dhidi ya Dawa za kulevya Nchini kuhakikisha vijana wanakuwa salama na kuokolewa kutoka kwenye uraibu wa matumizi ya dawa hizo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Mhe. Jenista Mhagama wakati akitoa taarifa Bungeni Jijini Dodoma kuhusu ufafanuzi wa hoja ya Mbunge wa Viti Maalum Mhe. Esther Bulaya akichangia kuhusu mapambano ya dhidi ya Dawa za kulevya Nchini.

Mhe. Jenista amesema kwa mujibu wa mikataba ambayo nchi imeridhia na kukubaliana Kimataifa katika kupambana na kuzuia dawa za kulevya ni pamoja na kushirikisha wadau mbalimbali kwa kuziwezesha nyumba za utengamao (Sober house) zinazoanzishwa na wadau.

“Kila mwaka wa fedha Serikali imekuwa ikitenga bajeti ya kuzisaidia hizo Sober house ili ziweze kufanya kazi ya kuhudumia waraibu wa dawa za kulevya ili tuweze kuokoa jamii yetu irudi katika hali ya kawaida na kuendelea na shughuli zao za uzalishaji,”Alisema Mhe. Jenista.

Aidha alipongeza juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Sukuhu Hassan kwa kazi kubwa inayofanywa katika mapambano hayo ikishirikiana na wadau ambao wamekuwa wakianzisha nyumba za utengamao.

About the author

mzalendo