Featured Kitaifa

TAMASHA LA SERENGETI 2022 NI FURSA YA UCHUMI KWA WANADODOMA- RC MTAKA 

Written by mzalendoeditor

Na. John Mapepele

Mkuu wa Dodoma. Mhe, Antony Mtaka amesema tamasha kubwa la kihistoria la Muziki la Serengeti linaloratibiwa na Serikali kupitia Wizara ya utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kushirikiana na wadau litakalofanyika jijini Dodoma  Machi 12-13, 2022 ni fursa pekee ya kiuchumi kwa wakazi wa Dodoma  na nchi nzima kwa ujumla.

Mhe. Mataka ameyasema haya leo Machi 4, 2022 ofisini kwake ambapo amefafanua kwamba tamasha hilo linatarajia kuwakutanisha zaidi ya wasanii mia moja wa muziki ambao watakuwa na mahitaji mbalimbali hivyo wakazi wa Dodoma watanufaika kwa kuwauzia bidhaa.

“Tunaishukuru Serikali yetu kwa kutusogezea wimbi la wasanii zaidi ya mia moja kwa mara moja   kwa kuwa tunakwenda kunufaika sana. Huu ni utalii wa kiutamaduni na kiuchumi, shime wanadodoma tutumie fursa hii adimu”. Ameongeza Mhe. Mtaka 

Aidha, Mhe. Mtaka  ameipongeza Wizara ya  Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa ubunifu wa kuongeza siku ambapo sasa litafanyika kwa siku mbili badala ya moja kama ilivyopangwa awali kutokana na mahitaji makubwa ya tamasha hilo kwa wasanii na wananchi.

Ametoa wito kwa wananchi wote wa Dodoma kushiriki  kikamilifu kwenye tamasha hili la kihistoria na kuwaomba wasanii wa Dodoma  kutumia tamasha  hili kujifunza  ili waweze kupiga  hatua zaidi katika  kazi zao. 

“Wasanii wa Dodoma jitokezeni kwa wingi ili kujifunza na kupata uzoefu kutoka kwa wanamuziki na wasanii wakongwe watakaotumbuiza kwenye tamasha hilo”. Amesisitiza  Mhe. Mtaka

Kwa upande wake, Dkt. Abbasi amesema kuwa Tamasha hili ndiyo tamasha pekee kubwa linalowaleta pamoja wasanii mbalimbali, wachanga na wakongwe, pia bendi za muziki kujumuika pamoja bila kujali lebo zao.

Ameeleza kuwa nia ya Serikali ni kuhakikisha wasanii wanabadilishana uzoefu kwenye fani ya muziki ili kukuza   vipaji vyao huku wakitumia tamasha hilo kutangaza utalii na vivutio mbalimbali vya Tanzania sasa inakwenda kufikiwa kwa ukamilifu.

About the author

mzalendoeditor